Kwa nini Kiebrania?

Kujifunza Kiebrania ni kwa Wasomi wa Utaalam tu, Sindiyo?

Kwa watu wengi, kujifunza lugha za kibiblia ni kama kuwa kuhani — kitu ambacho hawawezi kufikiri kukifanya, lakini wanajua kwamba watu wengine wanajisikia kuitwa hivyo. Kwa maneno mengine, watu wengi wanafikiria kuwa kujifunza Kiyunani na Kiebrania sio kwa mtu wa kawaida. Na baada ya miaka, watu walianza hata kufikiria kwamba wachungaji hawahitaji sana kusoma lugha za kibiblia.
 
Swali ambalo ninataka kuuliza ni: tulifikaje hapa katika historia ambapo tunadhani lugha za kibiblia ni kwa wakuu wa kiroho na wasomi? Sababu kuu tatu: 1) njia za kufundisha zinazoogopesha, 2) teknolojia isiyotosha, 3) gharama. Wacha tuelezee zaidi sababu hizo moja moja:  
 
  1. Tangu Zama za Kati (kama mwaka 400 BK hadi mwaka 1500 BK), watu wengi wamefundisha Kiebrania kwa njia inayoitwa “njia ya sarufi.” Njia hii inaifanya lugha kuwa kama mwandiko wa fumbo ambalo unapaswa kujifunza kulifafanua, badala ya kitu unachotumia na kufurahia. Kwa njia hii ya sarufi, unajulishwa haraka mipangilio migumu ya lugha ambayo unapaswa kujifunza kupitia kukariri kwa kichwa tu. Kwa mitazamo mingi ni kama kuna na kufanya hesabu. Kwa maneno mengine, njia hiyo sio kama njia uliyojifunza kuzungumza lugha yako ya mama ukiwa mtoto. Kwa watu wengi, inaogopesha sana, kwa hivyo wanawaachia “wataalamu” kusoma lugha za kibiblia.
  2. Kwa teknolojia isiyotosha kwa karne nyingi hakukuwa na njia ya mtu mmoja kufundisha mamilioni ya watu (kama unavyoweza kwenye YouTube leo). Ungeweza kuchapisha kitabu kinachofundisha watu, lakini kwa sababu bado kusoma lugha za kibibilia kunaogopesha, watu wengi wasingenunua kitabu chako, na ikiwa wangenunua, wangeishia kutokikutumia hawatakitumia. Lugha hufundishwa vizuri zaidi na mwalimu ambaye anakuonyesha jinsi ya kutumia lugha, ili uisikie sana, uone inavyotumiwa, na upate kuelewa jinsi lugha inavyofanya kazi. Huwezi kufanya hivyo na kitabu. Si shida hiyo tu, shida nyingine ni kwamba vitabu vinavutia tamaduni za fasihi andishi, sio tamaduni za simulizi. Na 70% ya tamaduni za ulimwengu ni za simulizi. Hiyo inamaanisha kwamba Wakristo wengi ulimwenguni hawatokei katika utamaduni ambao watu wanazoea kujifunza kupitia vitabu. Yesu aliishi katika utamaduni simulizi, ndiyo sababu alitumia muda mwingi kuzungumza na watu badala ya kutoa vitabu.
  3. Ni katika miaka 150 iliyopita tu vitabu vimekuwa nafuu kununua kwa watu wa kawaida wanaoishi katika tamaduni za kusoma na kuandika kama ulimwengu wa magharibi. Lakini katika sehemu zote nyingine ulimwenguni, vitabu ni ghali kwa mtu wa kawaida. Ikiwa watahifadhi akiba ya kununua kitabu, watanunua kitu ambacho hakiogopeshi (si kitabu cha sarufi ya Kiebrania!). Na mbaya zaidi: vitabu vya Kiebrania huelekea kuwa ghali zaidi kuliko vitabu vingine, na kwa kiasi kikubwa, havijatafsiriwa katika lugha nyingine nje ya ulimwengu wa magharibi. Kwa nini? Kwa sababu vitabu haviuziki vizuri katika tamaduni za simulizi! Kwa hivyo wengi wa Kanisa la ulimwengu wanaachwa bila chaguo la kujifunza Kiebrania kwa sababu ya umaskini wao, hawajui Kiingereza, na hawakukulia katika utamaduni wa kusoma na kuandika. Sijui kuhusu wewe, lakini hali hiyo inaonekana ni hali ya kutokuwa sawa.

Kukubali Mambo Yatakayokuja

Kwa hivyo sisi Aleph na Beth tunafanya kazi kwa bidii kutumia teknolojia mpya ambayo Mungu ametupa kufundisha Kiebrania kwa ulimwengu kwa njia inayowafaidisha zaidi. Kwa kuwa video zetu ni za kuona na kusikiliza, ni za kufurahisha, na za kuzamisha katika lugha, zinapendwa na watu kutoka tamaduni za simulizi. Sasa shida ya kuogopesha imepotea. Na kwa kuwa video ziko huru, na zitakuwa bure daima, hakuna kikwazo cha gharama. Mwishowe, kwa kuwa ni video za lugha moja, mtu yeyote katika kabila lolote anaweza kujifunza, bila kujua Kiingereza.

Kweli, Kujifunza Lugha Ni Kitu cha Kawaida

Sasa tunaishi katika ulimwengu ambao ni kawaida kujifunza lugha. Kuna mamia ya mamilioni ya watumiaji wanaotumia Duolingo ambayo ni moja ya programu maarufu za kujifunza lugha mbalimbali. Watu wengi duniani lazima watumie lugha mbili au zaidi katika maisha yao ya kila siku, na wamezoea kujifunza lugha mpya. Kujifunza lugha mpya ni kama kujifunza ujuzi wa aina nyingi ambao watu hufanya mara kwa mara. Hata Yesu na Paulo walijua lugha zaidi ya moja.

Kupiga chombo cha muziki ni ustadi mgumu kujua, kama kujifunza lugha, lakini mamilioni ya watu wa kawaida bado wanajifunza ulimwenguni kote. Kwa hivyo ikiwa watu wanatumia muda mwingi kujifunza vyombo vya muziki na lugha nyingine, kwa nini wasiweze kujifunza Kigiriki na Kiebrania? Inawezekana kabisa ikiwa tunasaidiana na kufanya ufundishaji bora upatikane bure!

Hatuishi Tena katika Zama za Kati

Teknolojia ya utunzaji muda imeruhusu watu wengi zaidi kuliko ilivyokua kujifunza vitu vipya. Elimu ilikuwa anasa kwa watu wa zama za kati, lakini sasa inawezekana kwa watu wengi zaidi ya hapo awali. Trilioni za masaa ya muda zitatumika kwa mambo mbalimbali kila mwaka. Kwa nini usitumie muda wako kujifunza lugha za Biblia?

Sisi sote tunajua kwamba tunapaswa “kukua katika neema na maarifa ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo” (2 Pet. 3:18). Kwa hiyo, kwa nini kujifunza lugha za Biblia kusiwe sehemu ya lengo la kukua katika maarifa hayo, ili kuisoma vizuri na kumwona Yesu zaidi?

Sababu Nyingine Kubwa

Tunaishi katika ulimwengu ambao unazidi kuchukia Biblia. Mafundisho ya uwongo ni tishio kubwa kuliko wakati wowote kwa sababu ya mtandao. Wale ambao hawana uwezo wa kupata lugha za asili wanaishia kuwa katika hatari ya mafundisho ya uwongo na kuweza kuchukuliwa na wale ambao wanapinga uaminifu wa Biblia.

Je! Ikiwa ungeona video kwa mtandao ya mtu akihubiri hivi: “Nimeangalia Kiebrania cha asili na kinasema kwamba wokovu wetu unategemea kiwango cha fedha tunachotoa!” Unapaswa kumwamini? Labda anahubiri na mamlaka inayoshawishi, amevaa suti ya kupendeza, na amesimama katika kanisa kubwa na maelfu ya watu wakisema, “Amina!” Tunawezaje kuwaelezea wengine kukosea kwake? Hatuwezi, kwa sababu hatujui Kiebrania. Kwa hivyo hatuwezi kumkabili juu ya uwongo anaohubiri, na hatuwezi kuzungumza kwa mamlaka yoyote kumuonya kaka yetu au dada yetu.

Hapa kuna jambo: watu wakizidi kujifunza lugha za kibiblia, waalimu wa uwongo hawataweza kuwadanganya. Yesu alisema, “Jihadharini na manabii wa uwongo, ambao huja kwenu wakiwa wamevaa mavazi ya kondoo lakini kwa ndani ni mbwa mwitu wakali” (Mt. 7:15). Na Paulo alionya: “Najua kwamba baada ya kuondoka kwangu mbwa mwitu wakali wataingia kati yenu, wasilihurumie kundi” (Matendo 20:29). Unafanya nini unapoona mbwa mwitu wanakaribia kula kondoo? Unatumia silaha. Ujuzi wa Kiyunani na Kiebrania ni moja wapo ya silaha zenye nguvu zaidi za kutetea watu dhidi ya mbwa mwitu wakali. Lakini vipi ikiwa kuna mtu mmoja tu katika kanisa lako lote ambaye ana silaha hiyo? Je! Ikiwa hayuko karibu wakati mbwa mwitu wanakuja? Wakiwa wengi watu walio na silaha katika Mwili wa Kristo, ndivyo mbwa mwitu watakavyokuwa na nafasi ndogo ya kuwaharibu kaka zetu na dada zetu. Ikiwa tunajua kwamba “Ibilisi huzungukazunguka kama simba angurumaye, akitafuta mtu wa kummeza” (1 Pet. 5:8) lazima tujiwekee silaha za Ukweli. Na tunapofanya bidii ya kujifunza lugha za Biblia tunaweza kupata hazina za thamani ambazo ni ukweli wa Mungu kwa hakika.

Kawaida Mpya

Hebu fikiria juu ya kitu kingine. Wakristo hutumia muda mwingi kusoma na kusikiliza maoni ya watu wengine juu ya Mungu. Wanaenda kwenye mikutano, hununua vitabu vingi, na hutumia masaa mengi kubishana na wengine juu ya tafsiri gani ni nzuri zaidi kuitumia. Ikiwa badala yake walitumia wakati wote huo na nguvu kujifunza lugha za Biblia, wangekuwa na vifaa vya kuwa wenye busara zaidi na wanyenyekevu, na kujua jinsi ya kujilisha wenyewe vizuri kiroho, badala ya kuwa wanyonge bila wengine kuwalisha.

Sisi sote tunajua msemo kwamba ni bora kumfundisha mtu kuvua kuliko kumpa samaki. Je! Ikiwa Wakristo walitumia wakati wao kuwasaidia wengine kujifunza lugha za Biblia bure, badala ya kuwaambia tu juu ya ufahamu wote mkubwa ambao walipata kutokana na kujua lugha za Biblia? Makanisa yetu yangekua kwa kina zaidi kiroho, watu wangeweza kuwawajibisha (hold accountable) viongozi wao kwa mafundisho mazuri, wazazi wangeweza kuwafundisha watoto wao vizuri, na watu wachache “wangepotea katika hadithi za uwongo” (2 Tim. 4: 4). Wacha tuanze harakati za kuifanya hii kuwa kawaida mpya. Kwa Mungu mambo yote yanawezekana!

Teolojia ya Kweli

Kijana anayeitwa Bitzer alisema, “Kadiri mwanatheolojia anavyojitenga na maandishi ya msingi ya Kiebrania na Kiyunani ya Maandiko Matakatifu, ndivyo anavyojitenga na chanzo cha teolojia halisi! Na teolojia halisi ni msingi wa huduma inayozaa matunda na inayokuwa baraka. ” Sisi sote tunahitaji teolojia halisi, na sisi sote tumeitwa kama sehemu ya mwili wa Kristo katika huduma yetu wenyewe inayozaa matunda. Wacha tusaidiane kupata vifaa tunavyohitaji kufanya huduma vizuri!

Kwa hivyo wacha tukubali kufanya jambo jipya: hebu tuache kukosoa tafsiri za Biblia, tuache kukosoa watu ambao hawajui teolojia sana au watu wasiokubali teolojia yetu. Tuache kukosoa madhehebu mengine, na tumia nguvu na wakati wote huo kujifunza lugha za Maandiko Matakatifu. Na hebu tujifunze kwa unyenyekevu, na “tuzidiane kwa kuonyesha heshima” (Warumi 12:10).

Uwatie Moyo Wengine

Nataka kusema kitu kwa wale ambao hawatajifunza Kiyunani au Kiebrania kwa sababu moja au nyingine. Watie moyo wale wanaojifunza! Wape moyo! Usiwacheke au uwaambie haijalishi! Wanapoleta Biblia ya Kiebrania kanisani usifanye mzaha juu yake! Mioyo yetu inajaribiwa sana kuwavunja moyo wale ambao wana vipawa tofauti au wale ambao wamepewa fursa tunazotamani tungekuwa nazo. Pinga jaribu hilo, na badala yake wakumbushe wale wanaojifunza kwamba masomo yao ni muhimu sana!

Na hii inaenea kwa Kanisa la ulimwengu. Wacha tufanye kila linalowezekana kuhamasisha kaka zetu na dada zetu ulimwenguni kote kujifunza na kukua! Hata ikiwa tunalazimika kutoa mchango ili kuwezesha kujifunza kwao kuwezekane, wacha tuhakikishe wana fursa sawa na sisi.

Kuna nukuu kutoka kwa Martin Luther ambayo imenitesa kwa miaka mingi:
Ni dhambi na aibu kutokujua kitabu chetu wenyewe au kuelewa masemo na maneno ya Mungu wetu; ni dhambi kubwa zaidi na upotevu kwamba hatujifunzi lugha, haswa katika siku hizi wakati Mungu anatoa na kutupa watu na vitabu na kila uwezo na ushawishi wa somo hilo, na Mungu anatamani Biblia yake iwe kitabu wazi. Loo, baba [wa kanisa] wapenzi wangefurahi mno kama wangekuwa na nafasi yetu ya kusoma lugha na kuja kusoma Maandiko Matakatifu baada ya kujitayarishwa hivyo! Ni kazi ngumu na bidii nyingi iliyogharimu wao kukusanya makombo machache, wakati sisi kwa nusu ya bidii – ndiyo, karibu bila bidii yoyote – tunaweza kupata mkate wote! Lo, jinsi bidii yao inavyoonyesha uvivu wetu na kututia aibu.
Mungu atuokoe kutoka kwa uvivu, na atutie moyo kufanya zaidi kwa ajili ya furaha yetu na utukufu wake.